Sunday, August 7, 2011

Naibu Waziri wa Fedha atembelea maonyesho ya nanenane mjini Dodoma

Ofisa Habari Ofisi ya Taifa ya Takwimu Doreen Makaya akitoa ufafanuzi jana kwa Naibu Waziri wa Fedha Pereira Silima juu ya umuhimu wa kitabu cha mapato na matumizi ya kaya binafsi kinavyoweza kumsaidia mwananchi kupanga bajeti yake vizuri kwa mwaka mzima na hivyo kuepuka matumzi yasiyo ya lazima. Naibu Waziri huyo alipata maelezo hayo wakati alipotembelea banda la Wizara ya Fedha kwenye maonyesho ya wakulima nanenane yanayofanyika kitaifa mjini Dodoma.
Naibu Waziri wa Fedha Pereira Silima(kulia) alipata maelezo jana juu ya mpango wa hiari kutoka kwaAfisa Masoko Mwandamizi James Mlowe(kushoto) alipotembelea banda la Wizara ya Fedha kwenye maonyesho ya wakulima ya nanenane ambayo yanafanyika kitaifa mkoani Dodoma.
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kazi na Ajira Edime Mangesho (aliyekaa kulia) akipata maelezo jana juu ya mafao mbalimbali yanayotolewa kwa wananchama wa Mfuko wa Pensheni (PPF) kutoka kwa Afisa Matekelezo wa PPF Julius Shayo(kushoto) wakati alipotembelea banda la Wizara ya Fedha kwenye maonyesho ya wakulima ya nanenane yanayoendelea mjini Dodoma.
Meneja Uhusiano wa Mfuko wa Pensheni(PPF) Lulu Mengele(kulia) akimweleza jana Naibu Waziri wa Fedha Pereira Silima juu ya idadi ya wananchama wa mfuko huo na mafao wanayotoa kwa wanachama wao wakati alipotembelea maonyesho ya wakulima ya nanenane mjini Dodoma.
Naibu Waziri wa Fedha Pereira Silima(kulia) alipata maelezo jana juu ya madeni ya ndani kutoka kwa Mhasibu aliyechini ya Idara ya Mhasibu Mkuu Wizara ya Fedha Huruka Mwinyigogo(kushoto) alipotembelea banda la Wizara ya Fedha kwenye maonyesho ya wakulima ya nanenane ambayo yanayofanyika kitaifa mkoani Dodoma.

Na Tiganya Vincent, MAELEZO-Dodoma

Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) imetoa Kitabu cha mapato na matumuzi ya kaya binafisi ili kuhakikisha wananchi wanapanga bajeti zao vizuri kwa ajili kudhibiti matumizi yao yasiyokuwa muhimu.

Ufafanuzi huo ulitolewa jana na Afisa Habari wa NBS Doreen Makaya jana mjini Dodoma alipokuwa akimweleza Naibu Waziri wa Fedha Pereira Silima juu ya umuhimu wa kitabu hicho katika kusimamia matumizi ya familia ya kila siku.

Alisema lengo la uandaaji wa kitabu hicho ni kumwelezesha kila Mtanzania kujenga tabia na mazoea ya kuweka kumbukumbu ya mapato na matumizi yake ya kila siku na kisha kujitathmini mwenyewe iwapo mapato yake yanalingana na matumizi yake.

Makaya aliongeza kuwa hatua hiyo ni muhimu kwani kila kaya itakuwa na fursa ya kujionea kama kweli waendelea na matumizi waliyonayo na pia kama kweli yanaweza kuwasaidia kuendelea kulingana mapato yao ya kila siku.

“Kitabu hiki kinampa kinamsaidia mtu kuweka kumbukumbu za kila kitu anachonunua au kupata na kisha anajipima kama kweli matumizi yake yanalingana na mapato yake… pia kinamtaka mtu hata unaponunua vocha aandike pia anapotoa ofa kwa mtu ni vema akaandika ili mwisho wa siku anajua ni kisia gani ametumia na je kinalingana na mapato yake ya siku hiyo?” alisema Afisa Habari huyo.

Alisema kuwa mtu akifanikiwa kukitumia kwa muda wa mwezi mmoja kinatamsaidia kubadili tabia yake kama alikuwa ana matumizi yanayozidi kiwango cha mapato yake atajirekebisha na kufikiria shughuli za maendeleo.

'Kitabu hicho kinamweleza mtumiaji kuandika kila kitu anachonunua kuanzia asubuhi hadi anapokwenda kulala na kisha kuangalia kama kweli kinawiana na fedha zake za siku ile' alisema Makaya.

Afisa huyo alisema kuwa hatua hiyo pia imaeanza kuwasaidia baadhi ya wanannchi ambao wameanza kutumia kitabu hicho kujiohoji kama matumizi yao ya kila siku yatawasaidia kujikomboa na umaskini.

Makaya alisema kuwa baadhi ya watu wamekuwa wakishindwa kufanya shughuli ujenzi wa nyumba na kusomesha watoto wao sio kwa sababu ya kukosa fedha bali kushindwa kupangia vema mapato na matumizi yao na hivyo kuwaona majirani zao wakifanya shughuli za maendeleo kwa kipato hicho hicho kidogo.

Hivyo alitoa wito kwa wananchi wanaohitaji kitabu hicho ambacho hutolewa bure kutembea Ofisi za Taifa za Takwimu kwa ajili ya kuelimishwa na kupata kitabu hicho kwa ajili ya kupata maendeleo yao na ya taifa.

Aidha aliongeza kuwa kuwa Ofisi hiyo ilitoa kitabu hicho ili kuwaandaa wananchi kutumia takwimu katika kupanga shughuli mbalimbali za maendeleo yao.

Kwa upande wa Naibu Waziri wa Fedha Pereira Silima alisema kuwa kutolewa kitabu hicho kitasaidia kutoa mwongozo kwa wananchi kujenga utamaduni kupangalia mambo yao na hasa mapato na matumuzi.

Aliongeza kuwa mwananchi atakapoelimika itakuwa rahisi kwake kuhoji juu ya matumizi mbalimbali ambayo sio ya lazima na hayamletee maendeleo.

No comments: