Monday, October 3, 2011

WANANCHI PEMBA WAFURAHIA SENSA YA MAJARIBIO YA WATU NA MAKAZI 2011

Karani wa Sensa ya Majaribio ya watu na makazi ya mwaka 2011 kutoka Ofisi ya Takwimu Pemba Bi. Time Juma Hamad akiuliza maswali na kujaza fomu za Dodoso wakati alipozitembelea familia mbalimbali eneo la Sizini wilayani Micheweni, Pemba kwa lengo kupima usahihi wa nyaraka,fomu na kumbukumbu mbalimbali zitakazotumika katika maandalizi ya sensa ya watu na makazi itakayofanyika nchi nzima mwezi Agosti, 2012.
Karani wa Sensa ya Majaribio ya watu na makazi ya mwaka 2011 kutoka Ofisi ya Takwimu Pemba Bi. Time Juma Hamad akiendelea na kazi
Wasimamizi wa sensa ya majaribio ya watu na makazi 2011 kutoka Ofisi ya Takwimu Pemba wakifuatilia maendeleo ya zoezi la ujazaji wa madodoso ya sensa katika maeneo mbalimbali wilayani Michweni Pemba wakiongozwa na Msimamizi mkuu wa zoezi hilo na Mkuu wa Ofisi ya Takwimu Pemba Bw. Haroub Ally Masoud (kulia).
Bibi Raya Ally Hamad mkazi wa eneo la Sizini wilayani Micheweni, Pemba akiwa na familia yake akitoa ushirikiano kwa kujibu maswali aliyoulizwa na mdadisi/karani wa sensa ya majaribio ya watu na makazi ya mwaka 2011 Bi. Time Juma Hamad (kushoto).

Na. Aron Msigwa –MAELEZO.Micheweni, Pemba.

Zoezi la Sensa ya Majaribio ya Watu na Makazi 2011 linalofanyika katika wilaya ya Micheweni,Pemba limeonyesha mafanikio makubwa baada ya wananchi kujitokeza na kushiriki kikamilifu kutoa taarifa mbalimbali zinazowahusu katika maeneo yao.

Msimamizi mkuu wa zoezi hilo ambaye pia ni Mkuu wa Ofisi ya Takwimu Pemba Bw. Haroub Ally Masoud amesema hayo leo mara baada ya kutembelea baadhi ya maeneo yaliyochaguliwa kwa ajili ya zoezi hilo wilayani humo.

Amesema maandalizi mazuri yaliyofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu yamelifanya zoezi hilo kufanyika kwa ufanisi mkubwa. “ Zoezi la sensa linaendelea vizuri, mpaka sasa hakuna kwikwazo ambacho tumekipata kutokana na mwitikio wa wananchi na ushiriki wao tunaoupata kutokana na elimu tuliyoitoa juu ya umuhimu wa sensa na upatikanaji wa takwimu sahihi kwa ajili ya maendeleo ya taifa”

Ameeleza kuwa serikali imeyachagua maeneo ya Sizini na Maziwang’ombe yaliyoko wilayani Micheweni kwa Pemba nzima kuwa maeneo ya majaribio kutokana na utaratibu maalum wa kitaalam uliotumiwa katika utafutaji wa takwimu kwa ajili ya mipango ya maendeleo.

Bw. Masoud amefafanua kuwa zoezi la utafutaji wa takwimu katika maeneo yaliyoainishwa linaendeshwa kwa ushirikiano kati ya karani na mtoa taarifa katika familia ambaye ni baba au mama na kuongeza kuwa maswali yanayoulizwa ni yale ya kawaida ambayo yanajibika kirahisi yakiwemo masuala yanayohusu uraia, shughuli za kiuchumi, vifo, hali ya nyumba zao na vifaa vilivyotumika kujengea nyumba hizo na upatikanaji wa huduma za jamii katika kaya husika.

Akifafanua kuhusu madhumuni ya sensa ya majaribio 2011 inayofanyika katika mikoa ya Arusha,Dar es Salaam,Kaskazini Pemba,Kigoma, Kilimanjaro, Manyara,Mara, Mjini Magharibi, Mtwara, Njombe na Pwani na kuzihusisha kaya 5000 inalenga kupima na kutathmini maandalizi ya sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012.

“Madhumuni ya sensa hii ya majaribio pamoja na mambo mengine ni kupima usahihi wa nyaraka na kumbukumbu mbalimbali zitakazotumika yakiwemo madodoso ,niongozo na fomu mbalimbali ” Amesema.

Aidha amebainisha kuwa utaratibu wa kuhesabu watu unaotumika katika sensa ya majaribio ndio huo huo utakaotumika katika sensa ya watu na makazi itakayofanyika nchi nzima mwezi Agosti mwaka 2012.

Kwa upande wake mmoja wa washiriki wa zoezi hilo ambaye familia yake ilishiriki zoezi hilo la majaribio Bi.Halima Komboisa amefurahia zoezi hilo na kueleza kuwa litatoa takwimu halisi juu ya maisha ya mtanzania.

“Natoa wito kwa watanzania wenzangu kushiriki kikamilifu katika zoezi hili la sensa ya majaribio ya watuna makazi kwani ni zoezi zuri,rahisi halina matatizo kwa upande wangu nimelipokea vizuri “ Amesisitiza Bi. Halima.

Naye diwani wa Wadi Bw.Ahmed Ally Mwinyi ameishukuru serikali kwa kuichagua wilaya ya Micheweni kushiriki zoezi hilo huku akisisitiza kuwa yeye kama kiongozi wa jamii kwa kushirikiana na viongozi wengine waliwaelimisha wananchi juu ya umuhimu na faida ya kuhesabiwa licha ya kuwepo changamoto chache walizokutana nazo wakati wa zoezi la uelimishaji.

No comments: