Saturday, April 21, 2012

Mimba zisizotarajiwa zinawaathiri wanafunzi wa kike kielimu


Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo
Mimba zisizotarajiwa ni miongoni mwa sababu zinazochochea wanafunzi wa kike mashuleni kunatokana na kupata mimba zisizotarajiwa.
Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo aliliambia Bunge jana alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Josephine Chagula (CCM).
Chagula alitaka kujua lini serikali itatenga za kujenga mabweni kwa ajili ya wanafunzi wa kike nchini kote.


Akijibu swali hilo, Mulugo alisema makazi stahili ya wanafunzi yanachangia kupunguza mdondoko shuleni, unaotokana na sababu mbalimbali likiwemo tatizo la mimba.
Mulugo alisema katika kuondoa tatizo hilo, awamu ya pili ya Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari imeweka mikakati ya ujenzi wa hosteli katika shule za sekondari.
Alisema serikali inatarajia kujenga hosteli 20 kwa mwaka zenye uwezo wa kulaza wanafunzi 48 kila moja.

Alisema wizara inaendelea kutoa stadi mbalimbali za maisha na ushauri nasaha mashuleni ikiwa ni sehemu ya kukabiliana na changamoto ya wanafunzi wanaopata mimba na kuwasaidia wanafunzi kuweza kujiamini.


Hatutajenga barabara ya Mnanila-Kasulu kwa kiwango cha lami
SERIKALI imesema haina mpango wa kujenga haina mpango wa kujenga barabara ya Mnanila-Kasulu kwa kiwango cha lami.
Kauli hiyo ilitolewa jana bungeni na Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe alipokuwa anajibu swali la Mbunge wa Manyovu, Albert Ntabaliba (CCM).

Mbunge huyo alitaka kujua ni  lini barabara ya Manyovu kutoka Mnanila hadi Kasulu itajengwa kwa kiwango cha lami.

Aidha, alihoji kama serikali haioni umuhimu wa kuunganisha barabara za mkoa wa Kigoma na mikoa mingine ili wananchi hao waweze kufanya shughuli za uchumi kama watu wengine nchini.
Akijibu swali hilo, Dk Mwakyembe alisema kutokana na ufinyu wa bajeti uliopo serikali haiwezi kujenga barabara hizo kwa kiwango cha lami.
Dk Mwakyembe alisema kipaumbele cha serikali kwa sasa ni kujenga kiwango cha lami kwa barabara kuu pekee.

Kuhusiana na kuunganisha barabara ya mkoa wa Kigoma na mikoa mingine, alisema ujenzi wa barabara ya Kigoma –Kidahwe inayoungaisha mikoa ya Kigoma, Tabora, Kagera, Shinyanga, Mwanza na Rukwa ilikamilika Juni 8 mwkaa juzi na iligharimu Sh. bilioni 33.7.


Kasi ya watoto wanaoishi mitaani inaongezeka 

SERIKALI imekiri kuwepo kwa ongezeko kubwa la watoto wanaoishi mitaani na ombaomba wanaokosa haki zao za kielimu na kiafya.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Haji Mponda, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Thuwayba Idris Muhammad (CUF).
Mbunge huyo aliihoji serikali kama ipo tayari kukubali kuwa imeshindwa kutatua suala la watoto wa mitaani na ombaomba.
Dk. Mponda aliliambia Bunge kuwa, kati ya watoto wanaoishi mitaani ni moja kati ya makundi ya watoto walio katika mazingira magumu.
Alisema takwimu za utambuzi wa watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi, uliofanyika katika halmashauri 95 hapa nchini zinaonyesha asilimia nne sawa na watoto 33,962 kati ya 849,054 walionekana kuishi kwenye mazingira magumu.

“Ili kukabiliana na hali hii serikali imeunda kikosi kazi kinachohusisha wadau mbalimbali wa masuala ya watoto,” alisema.


‘Mganga Mkuu awasilishe idadi ya wagonjwa ‘

MGANGA Mkuu wa wilaya ya Kisarawe ametakiwa kuwasilisha wizarani idadi ya watu ambao wanatibiwa kwenye hospitali ya wilaya hiyo.
Hayo yalisemwa jana bungeni na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Haji Mponda, alipokuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Kisarawe, Selemani Jafo (CCM).
Mbunge huyo alitaka kujua serikali ina mpango gani wa kuongeza idadi ya dawa kwa hospitali hiyo kukidhi idadi ya watu wanaokwenda kupatiwa matibabu hospitalini hapo.
Akijibu swali hilo, Dk. Mponda alisema Mganga huyo anatakiwa kuwasilisha majina hayo ili kuiwezesha wizara kuchukua hatua zinazostahili.
Kutokana na kukabiliana na  usumbufu wa dawa, vifaa, vifaa tiba na vitendanishi, alisema wizara imechukua hatua ya kusambaza dawa kwenye zahanati na vituo vya umma.
Dk. Mponda alisema wizara na Bohari Kuu ya Dawa (MSD), vinagawa dawa na vifaa tiba kwa kuzingatia vigezo mbalimbali vikiwa ni pamoja na idadi ya wananchi wanaopata huduma katika vituo vya umma.
“Hospitali za umma nchini ikiwemo hospitali ya wilaya ya Kisarawe zinapata mgao wa fedha za dawa, vifaa, tiba na vitendanishi kulingana na vigezo vilivyopo,” alisema

Alisema ili kurekebisha hali ya upatikanaji wa dawa, vifaa, vifaa tiba katika wilaya ya Kisarawe, Mganga Mkuu huyo ameagizwa kuwasilisha idadi ya watu wanaotibiwa hospitalini hapo.


Serikali inautambua mgogoro wa ardhi Mvomero - Mwanri

SERIKALI inatambua kuwepo kwa mgogoro wa ardhi baina ya mwekezaji na wakazi wa kitongoji cha Kinyenze katika wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro.
Hayo yalisemwa jana na Naibu Waziri wa, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mvomero, Amos Makalla (CCM).
Makalla alitaka kujua serikali inashughulikiaje mgogoro huo unaohusu uhalali wa umiliki mipaka na unyanyasaji mbalimbali.

Aidha, alihoji kwa nini kuna tofauti ya ramani ya sasa na ya awali ya mwaka 1950 kwa kuhusiana na mipaka. Akijibu swali hilo, Mwanri alisema mgogoro huo wa ardhi unahusu shamba Na. 296 lenye ukubwa wa hekta 97.8.


Wanawake hawajanufaika kielimu-Waziri

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba, ameliambia Bunge jana kuwa wanawake wengi hawajapata fursa ya kujiendeleza kielimu katika baadhi ya jamii.
Alisema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Susan Lyimo (Chadema) ambaye alitaka kujua serikali ina mikakati gani sasa inayotekelezeka ya kuwafaidisha walengwa.
Akijibu  alisema hilo, wizara yake kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imekuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha jamii kupiga vita mila na desturi kandamizi ambazo ni kikwazo katika kuendeleza wanawake.
Aidha alisema serikali imefanya jitihada kubwa katika kuhamasisha kuwaandikisha watoto wa jinsia zote shuleni bila ubaguzi na kuweka sheria ndogo. Vile vile serikali ilifungua shule za msingi kila kijiji na sekondari kila kata ili kuwawezesha watoto wote kupata elimu karibu na mazingira ya nyumbani.

Aidha, alisema wanawake wamekuwa wakijengewa uwezo kwa kupatiwa mafunzo ya ujasiriamali ili waweze kuendesha biashara zao kwa faida na kurejesha mikopo wanayopewa.


Milioni 936 zahitajiwa kwa umeme vijijini Mwibara

JUMLA ya Sh. milioni 936 zinatarajia kutumika kwa ajili ya kuviwekea umeme vijiji 12 vya Jimbo la Mwibara mkoani Mara.
Kauli hiyo ilitolewa jana bungeni na Naibu waziri wa Nishati, Adam Malima alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mwibara, Alphaxard Lugola (CCM).
Mbunge huyo alitaka kujua ni lini serikali itatekeleza ahadi ya Rais ya kuvipatia umeme vijiji vya Buzimbwe, Bulamba, Kasuguti, Mahyolo, Nyamitebili, Kasahunga, Namibu, Kitengule, Busambara, Bunere, Nambaza, Namsimo, Mwitende, Makwa, Masahunga, Nambubi na Bwanza.
Akijibu swali hilo, Malima alisema kutokana na tathmini iliyofanywa na Shirika la Umeme nchini (Tanesco) kuhusu upelekaji wa umeme kwenye vijiji hivyo 12.

“Gharama hizi za zinahusisha ujenzi wa njia ya umeme msongo wa kilovoti 33 umbali wa km 14.3, ufungaji wa vituo 12 vya kupotezea umeme kwa wateja pamoja na ujenzi wa njia ya msongo wa volti 400 yenye urefu wa km 18,” alisema

Malima alisema umeme katika vijiji hivyo utatokea katika njia kubwa ya umeme inayotoka Bunda kwenda Ukerewe.
CHANZO: NIPASHE

No comments: