Tuesday, May 1, 2012

TAARIFA KUTOKA SHIRIKISHO LA SOKA TANZANIA (TFF) LEO. WAIPONGEZA SIMBA



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa timu ya Simba kwa ushindi wa mabao 3-0 ambao iliupata juzi (Aprili 29 mwaka huu) dhidi ya Al Ahly Shandy ya Sudan katika mechi ya Kombe la Shirikisho iliyochezwa Dar es Salaam.

Ushindi huo umetokana na ushirikiano uliopo kuanzia kwa wachezaji, benchi la ufundi, viongozi, wanachama wa klabu hiyo na Watanzania kwa ujumla.

Ni imani ya TFF kuwa Simba haijabweteka kwa ushindi huo na badala yake sasa inajipanga kwa ajili ya mechi ya marudiano itakayochezwa nchini Sudan ili kuondoa Al Ahly Shandy kwenye michuano hiyo na kusonga mbele.

TFF kama kawaida itaendelea kutoa ushirikiano kwa Simba ili kuhakikisha inafika mbali kwenye mashindano hayo, na ikiwezekana kuandikika historia ya kuwa timu ya kwanza ya Tanzania kutwaa Kombe la Shirikisho.

PAZIA LIGI KUU VPL KUFUNGWA MEI 5
Ligi Kuu ya Vodacom msimu wa 2011/2012 kuwania ubingwa wa Tanzania Bara itafikia tamati Mei 5 mwaka huu kwa bingwa kujulikana ambapo timu zote 14 siku hiyo zitakuwa uwanjani.

Klabu kongwe za mpira wa miguu nchini Simba na Yanga zitakutanisha timu zao katika mechi itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Nayo Oljoro JKT itakuwa mwenyeji wa Polisi Dodoma katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha na Ruvu Shooting itacheza na Villa Squad katika Mabatini, Mlandizi.

Mechi nyingine zitakuwa kati ya Coastal Union na Toto African itakayofanyika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, African Lyon na JKT Ruvu (Uwanja wa Manungu, Morogoro), Azam na Kagera Sugar (Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam) na Moro United na Mtibwa Sugar (Uwanja wa Jamhuri, Morogoro).

Kwa mujibu wa kanuni namba 4(2)(c) ya Ligi Kuu ya Vodacom, timu tatu za mwisho katika msimamo wa ligi zitashuka daraja. Tayari Moro United na Polisi Dodoma zimeshashuka, iliyobaki itajulikana baada ya mechi za Jumamosi ambazo zote zitaanza saa 10 kamili jioni.

MIKOA SITA YAOMBA UENYEJI LIGI YA TAIFA
Mikoa sita imeshaomba kuwa wenyeji wa Ligi ya Taifa itakayochezwa katika vituo vitatu tofauti. Ligi hiyo inayoshirikisha mabingwa wa mikoa inatarajia kuanza baadaye mwezi huu.

Kamati ya Mashindano ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inatarajia kukutana wakati wowote kupitia maombi hayo kabla ya kufanya uamuzi wa vituo na tarehe ya kuanza ligi hiyo.

Mikoa iliyoomba vituo ni Dar es Salaam, Kigoma, Lindi, Mara, Shinyanga na Singida.

No comments: