Tuesday, August 16, 2011

Kashfa kwa Ngeleja, Malima


WADAIWA KUPATA MGAWO WA SH 4 MILIONI KILA MMOJA KUTOKA FEDHA ZILIZOKUSANYWA NA JAIRO
Mwandishi Wetu
TUHUMA zilizosababisha kupelekwa likizo kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo zimezidi kupanuka na sasa Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja na Naibu wake, Adam Malima wanadaiwa kupokea sehemu ya fedha zilizosababisha mtendaji huyo kupewa likizo ili kupisha uchunguzi dhidi yake.


Jairo yupo likizo baada ya Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo kuanzisha uchunguzi dhidi ya tuhuma zilizotolewa bungeni kwamba aliwaandikia barua wakuu wa idara chini ya wizara yake ili watoe fedha kusaidia kupitishwa kwa bajeti ya wizara hiyo, fedha ambazo zinatafsiriwa kwamba zililenga kuwahonga wabunge.

Lakini wakati umma wa Watanzania ukisubiri hatima ya Jairo huku suala lake likiwa bado halijafikia mwisho, imebainika kuwa Ngeleja na Malima kila mmoja alinufaika na mgawo wa fedha hizo kwa kila mmoja kupewa kiasi cha Sh4 milioni, kwa maelezo kwamba ni fedha za kuwakirimu wageni.

Imeelezwa kuwa kiasi cha fedha kilichokusanywa na Jairo na kuingizwa katika akaunti ya Tanzania Geological Survey (GST), namba 5051000068 kwenye Benki ya NMB, Tawi la Dodoma ni Sh460 milioni na siyo bilioni moja kama ilivyodaiwa awali.

Hesabu kwamba fedha hizo zingefikia Sh1 bilioni ilitokana na barua iliyosomwa bungeni na Mbunge wa Kilindi (CCM), Beatrice Shellukindo ambayo ilikuwa ikibainisha kwamba fedha zilizoombwa ni Sh50 milioni, ambazo zikizidishwa kwa idadi ya idara na taasisi 21 zilizopo chini ya Wizara ya Nishati na Madini zinaleta jumla hiyo ya kiasi cha fedha.

Mwandishi wa gazeti hili aliona dokezo la Julai 16, mwaka huu la Mkurugenzi wa Mipango wa Wizara ya Nishati na Madini aliyefahamika kwa jina la I.H. Swai kwenda kwa Jairo likipendekeza kwamba Waziri na Naibu wake wapewe kila mmoja kiasi cha Sh4 milioni kwa ajili ya kuwakirimu wageni: “Hasa katika kipindi hiki cha Bunge la Bajeti.”

Dokezo hilo lilisema: “Kulingana na uzito wa kazi za Wahe. Waziri na Naibu Waziri, nashauri wapewe entertainment allowance ya Sh4 milioni kila mmoja, ili kuwawezesha kubalishana mawazo/kushauriana na wadau muhimu na wananchi wa majimbo yao, wanaofika Dodoma kuwaona kwa masuala mbalimbali ya maendeleo ya majimbo yao, katika kipindi hiki cha Bunge la bajeti.”

Dokezo hilo liliidhinishwa na Katibu Mkuu, Jairo Julai 18, 2011 kwa kuandika neno “Sawa” kisha kulisaini ikiwa ni kukubaliana na mapendekezo ya Swai na siku hiyo fedha hizo kiasi cha Sh8 milioni kililipwa kwa wahusika.

Hata hivyo, maelezo ya dokezo hilo yanatofautiana na yale yaliyo kwenye fomu iliyotumika kwa ajili ya kufanya malipo hayo ambayo inasomeka “Fomu ya Malipo ya Entertainment Allowance kwa ajili ya wajumbe kuwezesha uwasilishaji wa hotuba ya bajeti kwa mwaka 2011/12.”

Chini ya kichwa hicho kuna neno tarehe........ ikiacha nafasi wazi kwa ajili ya kujaza tarehe ambayo malipo hayo yalifanyika na katika fomu ya malipo ya Ngeleja na Malima imeandikwa 18/7/2011.

Kwa mujibu wa fomu hiyo ya malipo, waliochukua fedha hizo Julai 18, 2011 ni wawakilishi wa viongozi hao ambao mmoja ametakwa kwa jina moja la Massola kwa niaba ya Ngeleja na mwingine aliyefahamika kwa jina la E. Shija aliyesaini fedha hizo kwa niaba ya Malima. Msaidizi wa Waziri Ngeleja anaitwa Sosthenes Massola, wakati msaidizi wa Malima anajulikana kwa majina ya Emmanuel Shija.

Julai 18, mwaka huu ni siku ambayo Serikali kupitia kwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda iliamua kuiondoa bungeni Hotuba ya Bajeti ya Nishati na Madini baada ya wabunge karibu wote waliopata fursa ya kuchangia kukataa kuunga mkono, hadi iliporejeshwa bungeni Agosti, 13 mwaka huu na kupitishwa baada ya Serikali kuwasilisha mpango wa dharura wa kukabiliana na tatizo la umeme nchini.

Bajeti ya wizara hiyo iliwasilishwa bungeni Ijumaa, Julai 15, 2011 na wabunge wengi waliopata nafasi ya kuchangia walieleza wazi kwamba hawako tayari kuiunga mkono kutokana na sababu mbalimbali zilizokuwa zikigusa sekta za madini na umeme.

Taarifa za awali za kiuchunguzi zilidokeza kuwa siku moja baadaye (Jumamosi, Julai 16, 2011) na Jumatatu Julai 18, 2011 kilichukuliwa kiasi kikubwa cha fedha kutoka katika akaunti ya GST, hali iliyozua maswali kuhusu mtiririko huo wa utoaji wa fedha.

Akaunti hiyo ndiyo iliyotumika kukusanya fedha kutoka katika taasisi mbalimbali zilizoko chini ya Wizara ya Madini kwa ajili ya kile kilichodaiwa kuwa ni kwa ajili ya kufanikisha uwasilishaji wa bajeti ya wizara bungeni.

Uchukuaji wa fedha nyingi ulizua hoja na wasiwasi kwamba huenda madai kwamba hakukuwa na nia njema ya matumizi ya fedha hizo yalikuwa ya kweli.

'Wachunguzi wetu wanajenga hoja hapa kwamba kwa nini fedha hizi nyingi zilichukuliwa Jumamosi baada ya mambo ya wizara kuonekana kuwa siyo mazuri siku iliyotangulia (Ijumaa)?,' kilihoji chanzo chetu na kuongeza kuwa:

'Hata hizi fedha nyingine zilizochukuliwa Jumatatu nazo zina walakini, lazima hapa tuchunguze kwa sababu kuna kitu ambacho siyo cha kawaida.'

Kwa mujibu wa nyaraka zilizopo, shughuli za kibajeti ni pamoja na posho za vikao (sitting allowance), posho za kujikimu (per diem), ununuzi wa vyakula na vinywaji na gharama za mafuta kwa magari ya watumishi hao.


Ngeleja na Malima

Ngeleja na Malima walipoulizwa kwa nyakati tofauti bungeni Dodoma jana kuhusu madai ya kupewa posho hizo, hawakuthibitisha wala kukanusha.

Ngeleja kwa upande wake alisema asingeweza kuzungumzia suala hilo kwani kwa kufanya hivyo ni kama angekuwa “akijitetea” hivyo kutaka suala hilo aulizwe Mkurugenzi wa Mipango ya Wizara yake na Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini.

“Mimi nadhani uwaambie watu wenu wa Dar es Salaam waende pale kwa Mkurugenzi wa Mipango, pale ofisini kwetu ili waweze kupata maelezo, yeye (mkurugenzi) na mhasibu mkuu ndiyo wanaofahamu haya mambo ya posho,” alisema Ngeleja.

Kwa upande wake, Malima alisema suala la msingi ni gazeti hili kufutilia suala la posho za mawaziri na manaibu wao katika Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma, ili kubaini iwapo wao ndiyo waliolipwa fedha za aina hiyo tu au pia ni kwa mawaziri wengine.

“Mimi nadhani mnatakiwa kuwauliza watu wa Utumishi ili wawaambie maana hapa tunapokuwa bungeni, kuna mambo mengi yanafanyika, sasa ni vizuri mkauliza ili mfahamu waziri na naibu wake ni stahili zipi wanazopaswa kupewa kama allowances (posho),” alisema Malima na kuongeza:

“Maana mnapaswa mjue na muusaidie umma wa Watanzania katika haya mnayoyaandika, kwamba hata kama tulichukua posho hiyo msingi wake ni nini? Halafu jingine kwani ni sisi tu au ni utaratibu wa Serikali kwa mawaziri wake?”

Mhasibu mkuu afafanua
Akizungumzia suala hilo, Mhasibu Mkuu wa Wizara hiyo, Rose Waniha alisema kuna taratibu zinazotumika katika kutoa posho hizo za kujikimu kwa waziri, naibu na katibu mkuu wawapo katika shughuli maalumu hasa vikao vya Bunge.Waniha alisema kiutaratibu, wakuu wa idara huwa wanafahamu kiasi cha fedha hizo za kujikimu kutegemea aina ya kazi za kiofisi.

'Kwa hiyo hata kunapokuwa na vikao bungeni mtu anayehusika anaangalia labda kila siku waziri au naibu anapaswa kupata kiasi gani cha fedha. Inawezekana ikawa Sh500,000 kwa ajili ya kukirimu wageni . Kwa hiyo hilo dokezo unalolizungumzia ninavyofahamu litakuwa ni la siku za vikao siyo siku mbili ndiyo zilipwe Sh4 milioni kwa mtu mmoja,' alisema.

Alipoulizwa kama kuna utaratibu rasmi wa kutoa fedha hizo za kukirimu wageni na viwango maalumu, alisema hakuna viwango maalumu vilivyomo katika dokezo lolote zaidi ya watu wa idara kuangalia uzito wa kazi na idadi ya wageni.

Kuhusu posho ya siku ya kawaida, alisema kwa kawaida waziri, naibu au katibu mkuu anapokuwa safarini, posho ya siku ni Sh80,000 lakini ni tofauti na fedha hizo za kukirimu wageni.

'Posho na fedha hizi za kukirimu wageni ni vitu viwili tofauti. Posho anazolipwa waziri au naibu ni Sh80,000 kama kawaida lakini pesa nyingine za kujikirimu hazina uhusiano na posho,' alisema.

MWANANCHI

No comments: