Tuesday, December 13, 2011

HOT NEWS....ASKARI WAWILI RUKWA WAFUKUZWA KAZI KWA WIZI


IGP Said Mwema


Na Francis Godwin
POLISI mkoani Rukwa imewafukuza kazi askari wake wawili na kuamuru wafikishwe mahakamani kwa kumwachia huru mtuhumiwa waliyemkamata akiwa na nyara za Serikali zenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 144. Nyara hizo ni meno 17 ya tembo.

Mwandishi wa mtanado huu kutoka Rukwa anaripoti kuwa ,Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Isuto Mantage, alisema jana kuwa Polisi imetoa adhabu hiyo baada ya kuridhishwa na ushahidi uliotolewa katika Mahakama ya Kijeshi kutokana na makosa mawili yaliyokuwa yakiwakabili askari hao wenye cheo cha Konstebo, waliofahamika kwa majina ya Fredrick na Venance.

Aliyataja makosa yao waliofikishiwa katika Mahakama ya Kijeshi kuwa ni kutotoa taarifa za uhalifu kwa viongozi wao na kumwachia mtuhumiwa waliyemkamata na nyara hizo za Serikali.

Pia kwa mujibu wa Mantage, mtuhumiwa mwingine ni askari wa kike mwenye namba 7593, Konstebo Salome ambaye alipewa barua ya onyo kali kwa kosa la kutotoa habari kwa viongozi wake.

Kamanda Mantage alisema askari hao walitenda kosa hilo Novemba 11, mwaka huu, saa tano usiku wakati wakiwa zamu katika chumba cha mashitaka katika Kituo Kikuu cha Polisi Wilaya ya Mpanda ambapo walipokea taarifa kutoka kwa raia wema kuwa kwenye gari liitwalo Adventure Connection linalofanya safari kati ya Mpanda na Kigoma, kuna abiria amebeba mzigo wa meno ya tembo.


Alisema kutokana na taarifa hiyo, askari hao bila kumjulisha kiongozi wao yeyote, walikwenda eneo la tukio na kumkamata mtuhumiwa huyo pamoja na meno ya tembo, lakini katika mazingira ya kutatanisha wakati wakiwa njiani kumpeleka kituoni, walimwachia na kuendelea na kazi bila kutoa taarifa kwa kiongozi wao.

Alisema siku iliyofuata, Ofisa Wanyamapori Wilaya ya Mpanda aliyefahamika kwa jina moja la Mushi, alipata taarifa kuwa ndani ya basi hilo lililokuwa limeanza safari kwenda Kigoma, kuna abiria amebeba meno ya tembo, hivyo aliwatuma askari kufukuzia basi hilo na kulikuta Mishamo umbali wa kilometa 140.

Inadaiwa kuwa polisi hao walifanya upekuzi katika gari hilo na kukuta vipande 13 vya meno ya tembo vikiwa kwenye begi moja lililokuwa kwenye buti la gari hilo na walipohojiwa abiria ili kujua mmiliki wa begi hilo, hakuna aliyejitokeza hivyo iliwalazimu askari hao kumkamata mhudumu wa gari hilo aliyekuwa na jukumu la kupakia mizigo kwenye buti la gari hilo.

Hata hivyo, uchunguzi wa shauri hilo ulipofanyika iligundulika kuwa siku moja kabla, askari hao wawili walikuwa wamepata taarifa na kumkamata mtuhumiwa aliyekuwa na nyara hizo na kisha kumuachia katika mazingira ya utata.



Askari hao walipokamatwa na kuhojiwa walikiri kumkamata mtuhumiwa huyo. Inasemekana kuwa wakiwa katika harakati za kumfikisha kituo cha Polisi, mtuhumiwa huyo aliyekuwa na meno manne ya tembo aliwatoroka na kukimbilia kusikojulikana.



Askari hao walishindwa kutoa maelezo ya kuridhisha kwa nini hawakutoa taarifa kwa wakuu wao, lakini walipopekuliwa katika nyumba wanazoishi, walikutwa na vipande vinne vya meno ya tembo ambavyo ukilinganisha na vile vilivyokutwa kwenye gari, vilionekana kuwa sawa na kufanya idadi yake kuwa 17.

Hata hivyo imebainika kuwa tembo sita waliuawa. Katika tukio jingine, Polisi mkoani Rukwa inamshikilia mtumishi wa benki ya NMB Tawi la Sumbawanga kwa tuhuma ya kuiba zaidi ya Sh milioni 35, mali ya wateja wa benki hiyo.

Kwa mujibu wa Kamanda Mantage, mtumishi huyo Harry Luvanda (31) anadaiwa kutenda kosa hilo kwa vipindi tofauti kati Januari hadi Novemba mwaka huu.

Alisema fedha hizo zinazodaiwa kuibwa kutoka kwa wateja mbalimbali kisha kuingizwa kwenye akaunti za wastaafu na wengine ambao ni marehemu waliokuwa watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga.



Inadaiwa kuwa fedha hizo huwekwa katika akaunti za watumishi hao kama mishahara yao kisha baadaye mtuhumiwa huyo huzichukua fedha hizo katika mazingira ya kutatanisha.


Mtuhumiwa huyo anakabiliwa na makosa tisa yakiwamo ya udanganyifu, kughushi na wizi akiwa mtumishi na benki na atafikishwa mahakamani wakati wowote kuanzia sasa.

No comments: