Saturday, April 7, 2012

BASATA INAUNGANA NA WATANZANIA WOTE KATIKA MAOMBOLEZO YA MSIBA WA KANUMBA…!!


BASATA inaungana na familia za wafiwa na wasanii wote nchini kwa maombolezo  ya msiba huu mkubwa na wa kihistoria.  Kufiwa na msanii huyu mahili kwenye tasnia ya filamu ni pengo kubwa kwa familia, Sekta ya sanaa na Taifa kwa ujumla kutokana na ukweli kuwa, aliweza kuutangaza utamaduni na sanaa yetu nje ya mipaka.

Kanumba atakumbukwa kwa moyo wake wa kujituma na kuthamini kazi ya Sanaa toka akiwa Kundi la Maigizo la Kaole ambapo moyo wake huo ulimfanya awe miongoni mwa wasanii walioleta mageuzi kwenye tasnia ya filamu kwa kuifanya kuanza kupendwa na wadau wengi zaidi.

Aidha, atakumbukwa kwa juhudi zake za kuinua vipaji vichanga katika tasnia ya filamu ambapo mara kadhaa katika kazi alizoziandaa alishirikisha wasanii wachanga ambao BASATA inaamini watakuja kuwa hazina kubwa kwa taifa letu.

BASATA linatoa pole kwa familia ya marehemu na Wasanii wote katika kipindi hiki kigumu. Ni vema wasanii wote tukatumia kipindi hiki kutathimini kwa pamoja michango yetu katika kukuza sekta ya Sanaa ikiwa ni pamoja na kuimarisha umoja wetu lakini pia tukiyaenzi yale yote mema yaliyofanywa na Steven Charles Kanumba.

Mungu ailaze roho ya Marehemu Steven Charles Kanumba mahali pema peponi. AMEN

Sanaa ni Kazi Kwa Pamoja Tuikuze na Kuithamini.

Ghonche Materego

KATIBU MTENDAJI, BASATA

No comments: