Friday, April 20, 2012

`Mawaziri wezi wanyongwe`



  Wabunge wawasha moto
  Kisa wezi wa fedha za umma
  Mkulo, Chami, Mponda watajwa wazi
Bunge limechafuka. Baadhi ya wabunge wametaka mawaziri wafukuzwe, huku wengine wakitaka wezi wa fedha za umma wanyongwe mara moja.

Kila mbunge aliyesimama jana alionekana kuwa na uchungu kuliko mwingine kiasi cha kufanya mawaziri wanaokaa viti vya mbele bungeni kutokuamini kilichokuwa kikiendelea.




Miongoni mwa wabunge waliowasha moto huo jana ni pamoja na Mbunge wa Ludewa (CCM), Deo Filikunjombe, aliyesema mawaziri wengi wanaongoza kwa wizi wa fedha za umma kama inavyoonekana kwenye ripoti za kamati za kudumu za Bunge na ameahidi kuwasilisha ushahidi wake bungeni.


Jana jioni Filikunjombe, alimtaja wazi Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo, kuwa si mwaminifu na amekuwa akifanya mambo mengi kwa maslahi yake binafsi kama alivyosema uongo bungeni juu ya Shirika Hodhi la Mashirika ya Umma (CHC).


"Aliyekuwa kuwa mwongo siyo Mheshimiwa Zitto, bali ni Waziri Mkulo," alisema.


Mbunge huyo aliyekuwa anaongea kwa hisia kubwa alisababisha kimya kikubwa ndani ya Bunge na nyuso za mawaziri kuonekana kuwa na mshangao mkubwa.


Awali, Mbunge huyo ambaye pia ni Naibu Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), aliyasema hayo bungeni jana wakati akijibu hoja ya Waziri wa Viwanda na Biashara, Cyril Chami, aliyewataka wabunge wasishinikize kuondolewa kwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Charles Ekelege, bila taratibu kufuatwa.
Alisema ana ushahidi wa kauli yake na atakayetaka anaweza kutoa majina ya mawaziri hao mmoja baada ya mwingine.
Baada ya kauli ya mbunge huyo jana mchana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisimama na kumtaka mbunge huyo athibitishe kwamba mawaziri wote ni wezi wa fedha za umma ama afute kauli yake.
“Haiwezekani mawaziri wote wakawa wezi wa fedha za umma, kama mheshimiwa mbunge ana ushahidi aseme ama afute kauli yake, hii haiwezi kuwa kweli mheshimiwa Naibu Spika,” alisema Lukuvi ambaye ndiye Mnadhimu Mkuu wa Serikali bungeni.
Kufuatia maelezo hayo, Filikunjombe alisimama tena na kumweleza Lukuvi kuwa yeye hakusema kuwa mawaziri wote ni wezi wa fedha za umma, bali alichosema ni kwamba mawaziri wengi wanaongoza kwa wizi wa fedha za umma.
“Mheshimiwa Naibu Spika, sikusema kwamba mawaziri wote ni wezi, nimesema mawaziri wengi ndio wanaongoza kwa wizi wa fedha za umma, ushahidi wa nilichokisema ninao na nitautoa kama unahitajika kwa kutaja mawaziri hao,” alisema.
Kauli ya Filikunjombe ilikuja kufuatia kauli ya Waziri Chami aliyodai kuwa hamlindi Mkurugenzi Mkuu wa TBS bali anachofanya ni kufuata taratibu za serikali.
“Huwezi kumfuta kazi mteule wa Rais bila kufuata taratibu wala kuwa na ushahidi wa tuhuma zinazoelekezwa kwake, lazima taratibu zifuatwe na kama ripoti ya ukaguzi ya CAG itaonyesha kuna wanaohusika na wizi hapa nawahakikishia serikali itachukua hatua ama mimi mwenyewe nitajiuzulu,” alisema Chami.
Kuhusu mkanganyiko wa yeye kusema kwamba ripoti ya CAG haijatoka, Chami alikiri kuwa ripoti hiyo ilitolewa kwa baadhi ya wabunge na wengine hawakuwa nayo.
Ripoti hiyo inafuatia uchunguzi maalum uliofanywa na CAG kuhusu ukaguzi wa magari yanayokuja nchini kutoka nje ya nchi, ambapo baadhi ya wabunge wanadai kuwa kampuni zinazofanya ukaguzi huo ni hewa kwani hazipo nje ya nchi.
Alisema hata naibu wake, Lazaro Nyalandu alisema kwamba ripoti hiyo iko tayari kwa kuwa aliazima kwa mmoja wa wabunge, lakini Wizara ilikuwa haijapatiwa rasmi.
Chami alisema aliwasiliana na CAG kutaka kujua kama aliwasilisha ripoti hiyo katika wizara yake, lakini alimjibu kuwa waliitoa kwa baadhi ya wabunge na Spika tu.
“Ripoti hiyo ilitoka siku nyingi, kuna baadhi ya watu walikuwa nayo, lakini sisi mheshimiwa Spika hatukuwa nayo, sisi tulishtukia watu wanaanza kumshutumu Mkurugenzi Mkuu wa TBS kuhusu kampuni hewa kabla hata ripoti yenyewe haijatoka,” alisema Chami.

Mwaka 2010, wabunge wa Kamati ndogo ya Kamati ya Hesabu za Serikali (POAC), wakiongozwa na aliyekuwa Mbunge wa Mbarali (CCM), Estelina Kilasi, ilikwenda Singapore na China kukagua kampuni zinazokagua magari yanayoingizwa nchini, kwa niaba ya Shirika la Viwango TBS.

Baada ya wabunge hao kurejea nchini, walidai kuwa kampuni hizo ni hewa kwani katika nchi walizokwenda hawakukuta ofisi wala wawakilishi wa kampuni hizo.
Kutokana na madai ya wabunge hao, Februari 2012, Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG),  nayo ilituma wakaguzi kwa ajili ya kukagua ofisi za ukaguzi wa magari nje ya nchi zinazosimamiwa na TBS.
Hatua hiyo ilikuja baada ya kamati za POAC, Fedha na Uchumi na Kamati ya Hesabu za Serikali Kuu (PAC) kudai kuwa Mkurugenzi wa TBS, Charles Ekelege, aliwasilisha taarifa za uongo kwamba Tanzania ina ofisi ya ukaguzi wa magari nje ya nchi wakati siyo kweli.
CAG, Ludovick Utouh, alisema kutokana na tuhuma zenyewe kuhusisha nje ya nchi, ofisi yake inalazimika kutuma wakaguzi ili kufanya uchunguzi na kuhakiki ukweli kuhusu tuhuma hizo.
Januari 27, mwaka huu POAC na PAC zilibaini kuwapo kwa tuhuma hizo zilizoelekezwa kwa mkurugenzi huyo na kumtaka asimamishwe kazi ili kupisha uchunguzi dhidi yake.
Ripoti hiyo ya CAG ndiyo inasubiriwa kwa hamu kwani ndiyo itakayobainisha ukweli kuhusu nani muongo kati ya POAC inayoongozwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe au Mkurugenzi Mkuu wa TBS.
Ingawa kwa mujibu wa ofisi ya CAG, ripoti hiyo imeshakamilika, lakini haijawasilishwa rasmi serikalini wala bungeni kwa ajili ya kufanyiwa kazi.


MAWAZIRI ‘WACHARAZWA’

Wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wameungana na wa kambi ya upinzani kuwasulubu mawaziri kuwa wameshindwa kazi ya kuondoa kero za wananchi nabadala yake wanashinda wakizurura kwenye dili zao binafsi.

Wabunge hao ambao walikuwa wakichangia kwa hisia kali na jazba, walishauri viongozi wanaokutwa na hatia ya kuiba fedha za umma wakiwemo mawaziri wanyongwe hadi kufa au wauawe kwa kupigwa risasi ili iwe fundisho kwa wengine.

Walikuwa wakitoa michango yao kuhusu namna walivyochukizwa na ufisadi ulioainishwa kwenye ripoti za POAC, PAC ya Serikali za Mitaa (LAAC).

Baadhi yao walishauri upelekwe haraka bungeni muswada wa kunyonga watu wanaokutwa na hatia ya kuiba fedha za umma, badala ya kupeleka miswada isiyo na maana kila uchao.

HOJA YA KUTOKUWA NA IMANI NA SERIKALI
Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu, amewataka wabunge kuwasilisha azimio la kutokuwa na imani na serikali ili kuwaondoa mawaziri wote  kutokana na wizi mkubwa wa fedha za umma ulioonekana kwenye ripoti tatu za kamati za kudumu za Bunge.

“Wabunge wengi waliochangia wamesema madudu yanayofanywa na serikali, lakini sijasikia hata mbunge mmoja aliyesema tuwasilishe hoja ya kuindoa serikali, sina chuki na Waziri Mkuu Mizengo Pinda, ila mfumo huu uliojaa na unaolinda wezi wa fedha za umma,” alisema.
Alisema wabunge wana mamlaka ya kushinikiza kuwaondoa mawaziri ambao wameshindwa kudhibiti wezi wa fedha na mali za umma badala ya kulalamika kila mwaka.
Alisema kila mwaka ripoti za kamati hizo tatu na ile ya CAG zinaonyesha uozo wa serikali kwa kushindwa kudhibiti wizi wa fedha za umma, lakini cha kushangaza hakuna hatua zozote zinazochukuliwa.
“Ripoti hizi hazina tofauti na zinazoletwa hapa kila mwaka, hizi ripoti ni catalogue ya wizi wa fedha za umma, kwa miaka kumi hatujawahi kuona ripoti hata moja ya CAG imekuja hapa inasema fedha za umma ziko salama, kila mwaka ripoti inaonyesha wezi hatua hazichukuliwi,” alisema.
Alisema zamani watu walikuwa wakiogopa mali za umma kwa kuwa waliokuwa wakizifuja walikuwa wakichukuliwa hatua, lakini kwa sasa wanaoiba ndio wamekuwa wakionekana kama mashujaa.
Alisema wananchi ambao wamekuwa wakiwataja wezi wa fedha za umma ndio wamekuwa wakipata shida kwa kusakamwa na kufunguliwa kesi zisizo na msingi wowote.
“Tumelalamika sana ndugu wabunge sasa inatosha, lazima awepo mtu wa kuishika pembe serikali, nyinyi wabunge wa CCM tumieni wingi wenu kuiadhibu serikali, msitumie wingi wenu kwa ushabiki wa kisiasa nchi inaangamia, nawaomba wenyeviti wa kamati hizi tatu wakati wa kuhitimisha waseme kwamba hawana imani na serikali,” alisisitiza.

HAMAD RASHID: TUCHUKUE HATUA
Mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid, alisema Ibara ya 62 ya Katiba inawapa mamlaka wabunge ya kuiwajibisha serikali, hivyo badala ya kulalamika wanapaswa kuchukua hatua.

“Kama kushauri tumeshauri sana, tumeshalalamika sana. Sasa huu ni muda wa kufanya maamuzi, dharau ya mawaziri na kejeli imekuwa kubwa sana, wanafanya mambo bila kujali lolote sasa ombi langu wabunge wote tutumie uwezo wetu kuwawajibisha,” alisisitiza Hamad.

MDEE: TUACHE ITIKADI, TUWANG’OE

Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee, alisema wabunge badala ya kulalamikia madudu yanayofanywa na serikali wanatakiwa kutumia mamlaka waliyonayo kuwaondoa mawaziri hao waliochoka.

Alisema lazima wabunge watoe azimio la kuwaondoa mawaziri hao kwa kuwa hatua ya kulalamika kila siku imekuwa ikiwapa kiburi na kuwapuuza wabunge kwa kujua kuwa hawana cha kuwafanya.

 “Mawaziri wengi wamepata nafasi kwa ajili ya kuwatumikia wananchi, lakini wanatumia nafasi hizo kwa dili zao binafsi, wanafanya mambo ya ajabu, wanatumia nafasi walizonazo vibaya na kwa maslahi yao, tuache kulalamika lalamika na tuchukue hatua za kuwawajibisha,” alisema.

“Mfano dhahiri kwamba hawa mawaziri wamechoka ni hili suala la wananchi wa mashamba ya Mbarali kuwekewa sumu kwenye mashamba yao, hili suala si geni limezungumzwa humu mara nyingi miaka miwili imeshapita sasa, lakini Naibu Waziri wa Kilimo wakati analijibu juzi alijibu kana kwamba ni kitu kipya kisichojulikana, badala ya kusema serikali imechukua hatua gani ameshasahau anatoa ahadi mpya,” alisema.

“Hawa mawaziri wanalipwa mishahara, lakini hawafanyi kazi, sisi wabunge tuweke pembeni itikadi za vyama vyetu tuwe kitu kimoja tuwashughulikie maana tusipofanya hivyo wananchi waliotuchagua watatushangaa, katika mambo ya msingi tuache U-CCM na Uchadema hapa,” alisema Mdee huku akishangiliwa.

ZAMBI: CHAMA KIWAADABISHE

Mbunge wa Mbozi Mashariki (CCM), Erasto Zambi, alisema kwa mujibu wa ripoti hizo tatu za serikali ni kama fedha za umma zimegeuzwa shamba la bibi kwani licha ya ripoti hizo kuonyesha wezi, hakuna hatua zinazochukuliwa.

Alisema kwa namna ambavyo mambo ya serikalini yanaendeshwa ovyo, mawaziri wamechoka na aliwashauri kila mmoja ajipime na kuwajibika mwenyewe katika hali ya kiuungwana badala ya kusubiri kutimuliwa.

“Wana-CCM kazi yetu ni kusimamia serikali yetu twendeni kwenye chama tukafanye maamuzi magumu ,” alisema.

“Ukaguzi maalum umefanyika wilaya ya Kishapu bilioni sita zimetafunwa, Rombo na Kilosa kuna madudu ya ajabu, watu wamechota fedha za serikali kama zao, lakini cha kushangaza ingawa makosa haya yalitokea miaka minne watuhumiwa wote bado wako kazini,” alisema.

Alisema ukaguzi wa CAG, umeonyesha kuwa kuna Sh. milioni 320, zimetafunwa Wizara ya Mifugo, Sh. milioni 375 Wizara ya Fedha na Sh. milioni 212 Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, lakini wahusika wote wako kazini.

“Ukiiuliza serikali kwa nini watu hawa hadi leo wako kazini wanakwambia kwamba wanafanya uchunguzi, wanafanya uchunguzi gani zaidi ya ule aliofanya CAG kama siyo namna ya kuwalinda wezi hao, tumepita kwenye halmashauri zote zimejaa madudu hakuna hata moja iliyo safi,” alisema huku wabunge wakishangilia kwa kugonga gonga meza.

KEISSY AMOUR: WAZIRI CHAMI AFUKUZWE

Ali Keissy Amour (CCM), Nkasi, alisema ni vyema hotuba zinazotolewa na wabunge hao zikarekodiwa ili zipelekwa kwa Rais, Waziri Mkuu na Makamu wa Rais ili wajue uozo unaofanywa na wasaidizi wao.

Alisema inashangaza kuona wezi wa mabilioni ya fedha za umma wakichekewa wakati magereza yamejaa wezi wa kuku na mbuzi.

Alisema TBS ndiko kumejaa uozo wa kila aina, lakini watendaji hao wanalindwa na Waziri wa Wizara ya Viwanda na Biashara na Katibu Mkuu wake hivyo alishauri wote wafukuzwe kazi.

Mbunge huyo alishauri Katibu Mkuu wa Wizara hiyo achunguzwe uhalali wa mali alizonazo yeye na ndugu zake ili kubaini ufisadi unaofanyika kwenye wizara hiyo.

“Mheshimiwa Spika ninavyojua kazi ya uwaziri haisomewi, kila mtu hapa anaweza kuwa waziri, lakini wenzetu hawa wamechoka waondoke, unakuta waziri anakwenda mkoani na msafara wa magari 40, unamtisha nani, nani hajaona magari, watu kule vijijini wana shida ya maji, dawa, zahanati, shule na wengine hata mlo mmoja kwao shida wewe unaenda ziara kuwaonyesha mbwembwe za nini, tuache mzaha baadhi ya nchi watu wanapigana mapanga kwa sababu kama hizi,” alisema.

“Kuna siku mimi na kamati yangu ya PAC tulikuwa tunajadili moja ya ripoti mimi nilichoka mapema, nikamwambia mwenyekiti wangu Cheyo kuwa nakwenda kulala mapema, hata hivyo sikupata usingizi ilibidi nimeze dawa ili nilale maana mambo niliyoyaona kwenye ile ripoti ni ya ajabu na ya kutisha,” alisema.

“Kila siku mnatuletea miswada isiyo na maana kutupotezea muda, tuleteeni muswada wa kunyonga watu, tuseme mtu akiiba mali za umma anyongwe hadi kufa na naamini tukinyonga watu 10 tu itakuwa fundisho na mambo yatakwenda, kuna mtu kawaletea wananchi wangu mbolea feki huyu tusimkawize akijulikana tu hata kesho anyongwe,” alisema.

SERUKAMBA: MAWAZIRI WANADHARAU WABUNGE

Mbunge wa Kigoma Mjini, (CCM), Peter Serukamba, alisema mawaziri hao wanawaona wabunge wa ovyo wanapowakosoa hivyo dawa ni kwenda kwenye chama na kuweka mkakati wa kuwaondoa.

“Kila wizara imejaa mambo ya ovyo ovyo, wabunge wa CCM twendeni caucus tukafanye kazi, yetu bila hivyo mambo hayataenda maana serikali inalidharau Bunge hili. Tangu Bunge hili lianze kazi wabunge hatujafanya kazi yanayoendelea ndani ya serikali Mungu ndiye anajua, twende vikao vya chama waziri ambaye hawezi kazi tumwambie Rais amwondoe,” alisema.
CHANZO: NIPASHE

No comments: