Wednesday, December 21, 2011

Maalim Seif Sharif Hamad:Zao La Karafuu Lazima Lifanyiwe Utafiti

Makamu wa Kwanza wa Rais,Maalim Seif Sharif Hamad akipewa maelezo na mfanyakazi wa Kivukoni Online Company, Nuru Muro, wakati alipotembelea ofisi za Tume ya Sayansi na Teknolojia huko Kijitonyama.Picha na Salmin Said-Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais-Zanzibar
-----
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad ameitaka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kuelekeza nguvu zake katika kufanya utafiti wa zao la karafuu kuliwezesha listawi vizuri zaidi na kupata thamani kubwa zaidi katika soko la Kimataifa.



Maalim Seif amesema pamoja na karafuu kuwa ndio zao kuu la biashara Zanzibar, hadi sasa hakuna utafiti unaofanywa kuhusiana na zao hilo, na sasa tume hiyo mbali na maeneo ambayo tayari inasaidia kuyaendeleza, kama vile kilimo cha mwani na kituo cha kilimo Kizimbani, kuna haja iwe ikifanya utafiti wa zao la karafuu.



Makamu wa Kwanza wa Rais, alisema hayo jana alipotembelea ofisi za tume hiyo Kijitonyama Dar es Salaam, kuangalia shughuli za utendaji wa tume, pamoja na kuzungumza na wafanyakazi.


Alisema karafuu zinazozalishwa Zanzibar zina ubora wa juu zaidi, lakini hadhi na heshima hiyo zitaweza kudumishwa , iwapo kutakuwa na utaratibu wa kufanywa utafiti, ikiwemo wa uoteshaji wa zao lenyewe, masoko na njia bora za kulisindika kabla ya kuuzwa.


Alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeamua kutumia nguvu kubwa kuliimarisha zao hilo na hivi sasa kupita Shirika lake la Biashara (ZSTC) inatoa shilingi bilioni moja kila mwaka, kwa ajili ya kukuza maendeleo ya zao hilo.


Akizungumzia zao la mwani, Maalim Seif alipongeza hatua ya tume hiyo kuelekeza nguvu katika kuliendeleza, kwasababu kama ilivyo kwa zao la karafuu, mwani unachangia kipato cha wananchi wengi wa Zanzibar, ambao idadi kubwa ni akinamama.


“COSTECH mtusaidie katika utafiti wa karafuu, tunahitaji kuwa na taarifa za maradhi yanayolikumba zao hili, lakini pia namna ya kufanya packaging kuliongeza thamani, naomba tushirikiane mazao haya yana nufaisha wananchi wengi Zanzibar”, alisema Maalim Seif.


Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Tume hiyo, Hassan Mshinda alisema nia ya tume ni kuona inatoa mchango mkubwa katika kukuza maendeleo ya nchi, ikiwemo Zanzibar kwa kutumia utafiti na mbinu nyengine mbali mbali za sayansi na teknolojia.


Alisema hivi sasa tume hiyo tayari imetenga shilingi milioni 600 kwa ajili ya kukiendeleza kituo cha kilimo kilichopo enel la Kizimbani Zanzibar, kwa ajili ya kujenga maabara mpya, kuendeleza zilizopo, pamoja na kuweka vifaa kwa ajili ya kazi za utafiti.


Mbali na hilo, alisema kwamba tume hiyo kupitia Taasisi ya Sayansi za Baharini ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam iliyopo Zanzibar, inasaidia uendelezwaji wa zao la mwani,kwa nia ya kuliwezesha lioteshwe kitaalamu zaidi na kuweza kupata soko kubwa na hivyo kuwanufaisha wakulima.


Aidha, akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Mkuu Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Florence Turuka alisema kuna mwamko mkubwa wa taasisi binafsi na zile za serikali kufanya utafiti wa nyanja tafauti, jambo ambalo ni dalili njema katika kukuza maendeleo ya nchi.


Alisema baada ya kufanywa utafiti huo wanachohakikisha ni kwamba matokeo ya utafiti huo yanawafikia wananchi, ili waweze kuyatumia katika shughuli zao za kila siku za kimaisha.


Turuka alisema tume hiyo, pamoja na Wizara yake ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia itahakikisha inakuwa karibu zaidi na Zanzibar kufanikisha harakati zake za maendeleo, na katika kufanikisha azma hiyo tayari tume imepata ofisi Zanzibar katika eneo la Tunguu.

Habari na Khamis Haji.


No comments: