Monday, January 16, 2012

Ahadi ya umeme ya JK utata mtupu (gazeti mwananchi)


Neville Meena
AHADI iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete ya kupatikana kwa megawati 3,000 za umeme huenda isitekelezwe katika muda uliopangwa kutokana na kutofanyika kwa maandalizi ya kutosha.Akilihutubia Taifa kuukaribisha mwaka 2012, Rais Kikwete alisema tatizo la umeme nchini litakuwa historia katika muda wa miezi 18 ijayo kutokana na mpango wa Serikali wa kusafirisha gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam.

“Maombi yetu kwa Serikali ya China ya kupata mkopo wa kujenga bomba la kusafirisha gesi kutoka Mtwara na mtambo wa kuchakata gesi inayotoka Songosongo yamekubaliwa,” alisema Kikwete katika hotuba yake ya Desemba 31, mwaka jana na kuongeza:“Utekelezaji wake unatarajiwa kuchukua miezi 18 na gesi itakayoletwa inaweza kuzalisha mpaka Megawati 3,000 za umeme. Baada ya hapo kasi ya kuongeza umeme itakuwa kubwa zaidi na tatizo la upungufu wa umeme linaweza kuwa historia.

”Hata hivyo, imebainika kuwa hadi sasa Serikali ya Tanzania na China hazijasaini mkataba wa kifedha ili kupata mkopo wa Dola bilioni moja za Marekani (karibu Sh1.6 trilioni) ambazo zitatumika kugharamia ujenzi wa bomba hilo, hivyo kuzua wasiwasi iwapo ujenzi wa bomba hilo utakamilika katika muda uliopangwa.Makubaliano ya awali ya ujenzi wa bomba hilo yalisainiwa China Septemba 26, 2011 na Tanzania ikiwakilishwa na Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja.

Baadaye ilisainiwa mikataba mingine midogomidogo lakini, kikwazo hadi sasa ni mkataba wa fedha.Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo alisema hadi mwishoni mwa wiki jana, mkataba wa kifedha ulikuwa bado haujasainiwa lakini akasema taarifa alizonazo ni kwamba utasainiwa hivi karibuni.“Kweli bado hatujasaini mkataba huo ila niko informed (nina taarifa) kwamba majadiliano yako kwenye hatua nzuri na yakikamilika tutasaini,” alisema Mkulo.

Mkulo alisema majadiliano yanayoendelea yanawahusisha Makatibu Wakuu wa Wizara za Fedha na Uchumi, Nishati na Madini, maofisa wa Serikali ya China na wakala wa utekelezaji wa mradi huo kutoka nchi hizo mbili.“Ninachoweza kusema ni kwamba bado tuko kwenye ratiba, tunafahamu umuhimu wa kukamilika kwa hatua hii, lakini lazima tujiridhishe.”Mapema wiki iliyopita, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dk Servacius Likwelile alisema bado kuna maeneo machache ya majadiliano baina ya wataalamu wa Tanzania na China na kwamba yakikamilika mkataba huo wa kifedha utasainiwa.
www.mwananchi.co.tz

No comments: