Thursday, February 23, 2012

Mwanafunzi adaiwa kuishi na mke

John Gagarini, Kibaha
SAKATA la wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Mwanalugali, wilayani Kibaha limeibua mambo mapya baada ya kubaini kuwa mmoja wa wanafunzi wa shule hiyo ameoa na anaishi na mke.

Hayo yamebainika siku chache baada ya shule hiyo
kuwasimamisha wanafunzi 30 waliokuwa wakiunda vikundi vya Al-Qaida na Al-Shabab huku mmoja akituhumiwa kumpiga mwalimu wake.

Hivi karibuni zilitokea vurugu kati ya makundi ya wanafunzi wa shule hiyo baada ya kutofautiana na kusababisha kutishwa kwa mkutano wa wazazi na walimu.Pia imebainika kuwa wanafunzi wa kike ambao wako kwenye makundi hayo wakuwa wakijihusiha na masuala ya mapenzi na vijana hao.

Taarifa zaidi zimebainisha kuwa wanafunzi ambao wako kwenye makundi hayo wamekuwa wakikiuka taratibu za shule na wanapoadhibiwa wamekuwa wakijiunga na makundi hayo.

Pia imebainika kuwa wanapokuwa kwenye vijiwe ambavyo viko jirani na shule hiyo wamekuwa wakivuta bangi.

Moja ya wazazi ambao walihudhuria mkutano wa wazazi na walimu wa shule hiyo ambaye hakutaka kutajwa jina lake alisema vitendo hivyo, vimekuwa vikifanywa na wanafunzi hao na kwamba mmoja ana mke na mtoto mmoja.

"Huyu tunamfahamu kuwa ana mke na mtoto, na siku moja alitumia panga kutaka kuwapiga wenafunzi wenzake akidai kuwa wamemchongea kuwa yuko kwenye moja ya makundi hayo, je ataweza kusoma kwa mtindo huo," alisema mzazi huyo.

Alisema wanamfahamu vizuri mwanafunzi huyo na kusema kuwa hali ya mwanafunzi kuwa na mke ni jambo ambalo halifai kufumbiwa macho kwani kwa kigezo hicho asingestahili kuwa shuleni.

Moja ya walimu wa shule hiyo ambaye naye hakutaka kutajwa jina lake alisema baadhi ya wanafunzi wamekuwa
wakikiuka taratibu za shule ikiwa ni pamoja na kuharibu suruali na kuzibana maarufu kama ‘modo’ kwa wale wa kiume na wale wa kike kuvaa sketi fupi ‘kimini’.

"Kuanzia sasa mwanafunzi wa kiume atakayekuja na suruali ya kubana tutaichana mguu mmoja na wa kike tutaichana, je wazazi mnakubalina na hilo, kama kuna mzazi hakubaliani na hili aseme kwani moja ya vitu vinavyoharibu wanafunzi ni mavazi, mwanafunzi wa kike kikianguka kitu
chini ukimwambia aokote ni aibu alisema mwalimu huyo," alisema mwalimu huyo.

Kwa pamoja wazazi na wa wawanafunzi hao walikubalina kuwa endapo mwanafunzi atakwenda na nguo ambayo iko kinyume na sare za shule, zitaharibiwa ili kurejesha nidhamu kwenye shule hiyo.

Naye Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Aron Ndunguru alisema walimwita baba wa kijana anayedaiwa kuuoa, lakini baba yake alikanusha na kusema kuwa wanamsingizia mtoto wake.

Ndunguru alisema tangu kutokea kwa vurugu za wanafunzi wa vikundi hivyo, mwanafunzi huyo hajafika shuleni tangu mwaka jana na kwamba wanaendelea na uchunguzi.

Mwanachi

No comments: